Tandahimba. Umewahi kuona mzigo unavyoshushwa kwa kreni? Basi hivyo ndivyo alivyoshuka katika uwanja Kassim Majaliwa, Tandahimba mkoani Mtwara nchini Tanzania, mmiliki wa wimbo ‘Uno’ msanii kutoka Tanzania Harmonize maarufu Konde Boy.
Hii ni mara ya kwanza kwa staa huyo kufanya shoo akiwa nje ya lebo ya WCB, ambapo licha ya kiingilio kwa mashabiki kilikuwa Sh10,000 alijaza uwanja na aliimba na mashabiki wake mwanzo mwisho.
Akishuka uwanjani hapo usiku wa kuamkia leo Januari 1, 2020 kwa mashine kama zile zinazotumika kubeba mizigo, Harmonize alikuwa akiimba na mashabiki waliofurika uwanjani hapo wakipunga mkono kutoka upande mmoja kwenda mwingine.
Neno kuu aliloshuka nalo baada ya kuimba shairi moja lilikuwa ni ...Tandahimba...Tandahimba na mashabiki waliitikia, pamoja naye.
Akiwa amebananisha miguu pamoja, Harmonize aliacha kuimba na kushuka taratibu huku mashabiki wakishangilia kwa kusema ...Konde ...konde....
Mbali ya kushuka na kreni zinazotumika kushushia mizigo, pia nyota huyo alipanda juu ya mti na kutumbuiza akitokea huko huku mashabiki wakiimba naye na kupunga mikono juu.
Kutokana na wingi wa watu, wakati wanapunga mikono inaonekana kwa juu kama maua huku simu zao wakizitumia kupiga picha.