Dar es Salaam. Msanii kutoka lebo ya WCB, Rajab Abdul maarufu kwa jina la Harmonize, amempa zawadi ya gari msanii Q Chief.
Akizungumza na waandishi wa habari leo, Julai 22 ,2019 Harmonize amesema ameguswa na maisha anayoishi kwa sasa ya msanii huyo na kuona ana kila sababu ya kusaidiwa kuwa na usafiri.
Akieleza zaidi amesema hata leo alipokuwa akienda kwenye mkutano huo wa waandishi wa habari uliofanyika Hoteli ya Hyatt Regency, alitumia usafiri wa bodaboda na kumuomba amlipie atakopofika jambo lolomuumiza moyo.
Msanii huyo mkali wa kibao cha Niteke, Never give up, alienda mbali zaidi na kueleza kuwa Q Chief amekuwa kati ya msanii aliyemvutia kuingia kwenye muziki na kueleza siyo yeye tu wapo wengine wakubwa waliong'aa kupitia yeye.
"Leo mpaka unaona wasanii wanaendesha magari, wanamiliki majumba kutokana na muziki na moja ya watu waliowavutia na walikuwa ‘wakicopy’ nyimbo zao ni pamoja na Q Chief na mimi nilikuwa mmoja wapo niliyekuwa nikiandika hadi kwenye daftari," amesema.
Hata hivyo, amesema msaada huo haujaishia hapo kwani wametoa naye nyimbo tatu ambazo zinaachiwa leo saa 1:00 jioni na kuomba jamii impokee.
Pia Soma
- Kubenea ataka TCRA itoe taarifa kuhusu udukuaji
- VIDEO: Hapi awageukia wanaomhujumu Rais
- Iran yadai kukamata majasusi wa Marekani
Q Chief amesema hakuamini kama kuna watu wanamthamini kiasi hicho hadi kuamua kumpa gari.
"Nimejikuta nalia machozi ya furaha, kwani kitendo alichokifanya Harmonize ni cha kiungwana sana angeweza kuwasaidia wengine lakini naona anisaidie mimi," amesema msanii huyo.
Amesema pamoja na kutumia usafiri wa umma wakati maisha yake yameenda kombo anashukuru hakuwa akijisikia vibaya kwa kuwa hajawahi kuishi maisha ya kuigiza hivyo alikubaliana na kila hali.