Dar es Salaam.Mwanamuziki Harmonize anashikiliwa kwa zaidi ya saa tano katika kituo kikuu cha polisi jijini Dar es Salaam alipokwenda kujisalimisha akituhumiwa kuvuta kitu kinachotoa moshi alipokuwa nchini Ghana hivi karibuni.
Akizungumza na wasanii mwishoni mwa wiki, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda alisema ameagiza mwanamuziki huyo anayetamba na wimbo Paranawe achunguzwe baada ya kuweka picha inayomuonyesha akivuta kitu kinachotoa moshi.
Makonda alisema alimwagiza Gavana wa kule amchunguze alichokuwa akivuta na kama ikithibitika kilikuwa na kilevi angemwajibisha.
Makonda ambaye ni mlezi wa lebo ya WCB inayosimamia kazi za Harmonize, alisema kama mzazi angemwajibisha kwa kumweka ndani mwanaye iwapo itathibitika kuwa kilikuwa kilevi.
Leo Jumatano Februari 6, 2019 mwanamuziki huyo amejisalimisha katika kituo hicho akiwa amejifunika kichwani kwa kuvaa sweta jeusi na miwani.
Alipofika kituoni hapo alitimua mbio huku akiwafurusha waandishi waliokuwa wakijaribu kumpiga picha.
Soma Zaidi: Makonda atangaza kumweka rumande Harmonize