Dar es Salaam. “Hatuwezi kuwa wa kwanza kuachana wala hatuwezi kuwa wa mwisho.” Ndiyo kauli ya mwigizaji Florah Mvungi kuhusu ndoa yake na mwanamuziki H Baba anayodai ilivunjika miaka mitatu iliyopita.
Kwa mara ya kwanza, mwigizaji huyo aliyewahi kutamba na maigizo ya Bongo Dar es Salaam ameeleza kuachana na mumewe H Baba.
Mastaa hao walifunga ndoa mwaka 2013 na kujaaliwa kupata watoto wawili waliowapa majina ya Tanzanite na Afrika.
Akizungumza na Mwananchi, Florah amesema ndoa yao ilivunjika takribani miaka mitatu iliyopita lakini aliamua kukaa kimya kwa sababu ambazo hakutaka kuziweka wazi.
Kuhusu sababu za kuachana amesema: “Siwezi kusema nani alikuwa tatizo au nini kilikuwa chanzo, muhimu tu mashabiki wangu wajue we are no longer together (hatupo pamoja).”
Akizungumzia kuhusu maisha ya ndoa alikiri kwamba yana changamoto nyingi lakini akashauri wanawake wanapoona yanawashinda wasisite kutoka.
"Binafsi ninachoangalia ni amani ya watoto wangu, hivyo kila mtu ana maisha yake kwa sasa japokuwa nashukuru watoto wangu nakaa nao," amesema.