MENEJA wa muziki wa kizazi kipya, Saidi Fella amesema hakuwahi kuwa na ugomvi na mwanamuziki, Juma Nature ila makundi yanayomzunguka ndiyo yaliyowachonganisha wakidhani anapata fedha nyingi.
Akizungumzia kuhusiana na utendaji kazi wa mwanamuziki huyo alisema anaamini Nature bado ana nyota ya muziki, isipokuwa marafiki wa karibu wanaojiita wadau au matajiri ndiyo waliokuwa wakimshauri vibaya.
Alisema kwa zaidi ya miaka 10 amekuwa mbali na mwanamuziki huyo, ambapo kwa sasa ameamua kurudia tena kumsimama kazi zake akiwa kama mshauri na kumtaka kujiepusha na makundi yasiyokuwa na faida.
“Hata Diamond Platnumz nilimwambia kama unataka kufanya kazi na mimi, sihitaji makundi makundi watu ambao hawana faida,” alisema.
Kwa sasa mwanamuziki Juma Nature pamoja na Saidi Juma ‘Chege’ wamefanya kazi kwa pamoja chini ya Saidi Fella .