FAINALI ya shindano la Safari Lager Nyama Choma linafikia tamati kesho katika baa ya Govonors Pub, tukio litakaloendana na burudani za aina mbalimbali. Akizungumzia tukio hilo, Meneja wa Bia ya Safari, Pamela Kikuli amesema baa 60 kutoka Dar es Salaam zitashiriki katika shindano hilo.
Alisema shindano hilo linalenga kuwajengea uwezo wachoma nyama nchini kuandaa nyama katika ubora zaidi na kwa usafi. Pamela alisema bia hiyo imekuwa ikiandaa shindano hilo mara kwa mara.
“Lengo ni kuwa karibu zaidi ya wateja kama inavyofahamika bia inakwenda na nyama hivyo bia hii imeona kuna haja ya kuwafikia wachoma nyama hawa na kuwashindanisha,” alisema.
Alisema shindano hilo limeandaliwa kwa kuzingatia haki ambapo katika hatua ya awali kila baa majaji walipokuwa wakienda walikuwa wakipata wasaa wa kuzungumza na wachoma nyama wa baa husika.
Alisema licha ya kuwa mshindi atapatiwa Sh milioni mbili na kushiriki kilele cha tamasha la Nyama Choma litakalofanyika Desemba 4 na 5, washiriki wengine watapatiwa vyeti vya ushiriki.
Majaji wa shindano hilo ni Fred Uisso ambaye amewakilisha nchi katika mashindano ya kimataifa ya mapishi na kwa sasa anaandaa kipindi cha runinga cha Masapta Sapta. Mwaka 2016 alishinda shindano la dunia ya uchomaji nyama nchini Marekani.
Mwingine ni Hassanal Msiha ambaye ni mkufunzi wa Chuo cha Zanzibar Transworld Academy akijihusisha na masuala ya mapishi ana amejikita katika uokaji shughuli aliyoifanya kwa miaka saba. Pamela alisema baada ya Dar es Salaam, tamasha hilo litafuatia mkoani Kilimanjaro na litakuwa na utaratibu kama wa Dar es Salaam.