Dar es Salaam. Msanii wa Bongofleva nchini Tanzania, Godfrey Tumaini maarufu Dudubaya ameitwa na Baraza la Sanaa la Taifa (Basata) kwa ajili ya mahojiano.
Dudubaya anatakiwa leo Jumanne Januari 7, 2020 kufika ofisi za baraza hilo zilizopo Ilala Sharif Shamba, Dar es Salaam, Tanzania.
Hata hivyo, katika majibu yake, Dudubaya amesema ameuona wito huo lakini hataenda.
Badala yake amelitaka baraza hilo kabla ya kumuita kutatua migogoro iliyopo kati ya baadhi ya vyombo vya habari na wasanii ili muziki uweze kwenda mbele.
Katika barua iliyosainiwa na Kaimu Katibu Mtendaji wa Basata, Flora Mgonja imesema baraza limesikitishwa na kauli zisizokuwa na maadili wala staha kupitia video fupi zilizorushwa kwenye mitandao ya kijamii.
"Video hizo fupi zilizorushwa kwenye mitandao ya kijamii zinamuonyesha Dudubaya akitoa lugha zisizo na maadili.”
"Hivyo baraza linamtaka msanii huyo (Dudubaya) kufika bila kukosa katika ofisi za Basata zilizopo Ilala kwa ajili ya mahojiano zaidi.”
Mwananchi inaendelea kuwatafuta Basata ili kujua ni hatua gani zinapaswa kuchukuliwa zaidi endapo msanii atakaidi maagizo ya wito wao kwani simu zao zimekuwa zikiita bila kupokelewa.
Endelea kufuatilia Mwananchi kwa habari zaidi