Dar es Salaam. Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo nchini Tanzania, Dk Harrison Mwakyembe amesema kuanzia leo Jumatano Agosti 28, 2019 ndio mwisho wa kutumia kazi za wasanii nchini bila kulipia.
Dk Mwakyembe ametoa kauli hiyo leo katika mkutano uliowahusisha wasanii kujadili maslahi yao uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Katika maelezo yake Dk Mwakyembe amesema kila mtu anayetumia wimbo wa msanii au mfumo wowote unaotumia muziki wa wasanii wa Tanzania lazima wachangie iwe kwenye kumbi za starehe, mabasi na hotelini.
Amesema haiwezekani msanii anatengeneza wimbo na badala ya kulipwa wimbo huo ukipigwa redioni, yeye ndio anayelipia.
Huku akionyesha kusikitishwa na malipo ya wasanii nchini, Dk Mwakyembe amesema nchi nyingine ni ngumu kumsogelea mwanamuziki kutokana na ulinzi walionao.