Msanii Diamond Platnumz pamoja na bendi yake nzima watakonga nyonyo za wakulima wa Tumbaku wa wilaya ya Chunya mkoani Mbeya kupitia tamasha la 'sauti ya mkulima wakati ni sasa' lililoandaliwa na kampuni ya Mkwawa Leaf Tobacco Ltd yenye makao yake makuu mjini Morogoro.
Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Ahamed Huwel amesema tamasha hilo linalolenga kuhamasisha kilimo cha tumbaku wilayani humo na nchini kwa ujumla litafanyika Jumapili Mei 14, mwaka huu katika kata ya Lupatingatinga wilayani humo.
Pamoja na kuongeza hamasa ya kilimo hicho cha kibiashara kinachoweza kuinua uchumi wa wakulima na Taifa kwa ujumla, Huwel amesema tamasha hilo litatumika pia kutoa elimu ya madhara ya ajira za watoto mashambani ili wasikose haki zao ikiwemo ya elimu.