MSANII wa kizazi kipya, Naseeb Abdul ‘Diamond Platnumz‘ amesema hana kinyongo na wanamuziki wenzake wanaomuimba kwenye nyimbo zao iwe kwa wema au mabaya.
Diamond alitoa kauli hiyo baada ya baadhi ya wasanii wengi kila wakitoa nyimbo wamekuwa wakimtaja kwa ubaya, lengo likiwa kazi zao zipokelewe vyema sokoni na mashabiki. Akizungumza Dar es Salaam jana, Diamond alisema anaamini hizo ni baraka kutoka kwa Mungu, kwani amemfanya kuwa kioo, hivyo wanatumia ukubwa wake kutengeneza riziki.
“Kuna watu wako mtaani nao wanatamani waimbwe, wanatamani wasemwe vibaya, wengine wanafanya vituko kwenye mitandao ili tu waonekane, ikitokea wasanii wenzangu wananiona na wananitaja kwenye nyimbo zao kwangu ni Baraka kutoka kwa Mungu siwezi kuchukia.
“Mungu amenifanya kuwa kioo na nina nguvu kwa watu na wananikubali sitakiwi kununa watu wanaponizungumza kwa wema au ubaya kwa sababu wao ni binadamu wanatafuta riziki kupitia mimi nikichukia itaonekana namkasirikia Mungu kwa ukubwa na umaarufu.”
Diamond alisema alikuwa anapambana kuomba nafasi hiyo, ambayo Mungu amemjalia na amewaomba wasanii wenzake kuendelea na wafurahie uwepo wake.