Msanii wa Bongo fleva Naseeb Abdul, ‘Diamond Platnumz’ usiku wa kuamkia leo ameshinda tuzo za MTV EMA katika kipengele cha Best African Act na kuwakilisha vyema Watanzania.
Katika kipengele hicho, Diamond alishindanishwa na wasanii wakubwa wakiwemo Burna Boy na Asake wa Nigeria, Libianca kutoka Cameroon na Tyler ICU kutoka nchini Afrika Kusini.
Ushindi wa Diamond katikati ya mastaa hao wakubwa nchini Nigeria ni jambo ambalo halikutarajiwa na wengi na ndiyo maana baada kuibuka mshindi kuliibuka mjadala mkubwa katika mitandao ya kijamii.
Wengi wameoneshwa kufurahishwa na Diamond hasa kwa kuwaangusha miamba ya Nigeria, Asake na Burna Boy na kuwataka wasanii wengine kuiga mfano huo.
Kwa upande wa Wanaigeria, ushindi wa Diamond haujawafurahisha baadhi ya Wanigeria kuanza zengwe mitandaoni kwamba kulikuwa na figisu, jambo ambalo wenyewe kwa wenyewe walianza kupingana.