Nyota wa Afrobeat kutoka Nigeria, Davido ametangaza siku ya Jumanne kuwa atatoa dola 156,000 kwa yatima nchini humo.
“Mimi na wakfu wangu tunaahidi kutoa Naira milioni 300 kwa vituo vya yatima nchini Nigeria, ikiwa ni mchango wangu wa kila mwaka kwa taifa. Jinsi ya utoaji wa fedha nitatangaza kesho,” Davido ameandika kupitia mtandao wa X, siku ya Jumanne.
Davido, ambaye jina lake halisi ni David Adedeji Adeleke, katika miaka ya hivi karibuni amejiongezea umaarufu kwa mashabiki wake kutokana na shughuli za utoaji misaada.
Mwaka 2021, alikusanya Naira milioni 200 kutoka kwa marafiki zake na mashabiki wake baada ya kuandika kwenye mtandao wa X akiomba msaada ili akomboe gari lake la Rolls Royce kutoka bandarini.
Davido aliongeza Naira milioni 50 za kwake na kutoa msaada jumla ya Naira milioni 250 kwa yatima nchini Nigeria.
Mwaka uliofuata aliunda wakfu wa David Adeleke. Tangu wakati huo, Davido na wakfu wake wamekuwa wakitoa misaada kwa nyumba za watoto yatima nchini Nigeria kila mwaka.