RUTHA Bushoke, msanii wa muziki wa kizazi kipya amesema kuwa, Rais Dk John Magufuli alikuwa mtetezi wa wanyonge, hivyo kifo chake kimewaachia simanzi wengi.
Akimzungumzia kiongozi huyo jana, msanii huyo alisema kwa matendo ambayo alikuwa anayafanya wakati wa uhai wake aliwapa nafasi kubwa wanyonge kuishi kwa tabasamu, hivyo kuondoka kwake kumeacha huzuni kubwa ndani ya mioyo ya wengi.
“Ni wengi ambao alikuwa anawatetea na hakuna ambaye alikuwa haoni kazi yake aliyokuwa anafanya. Ukweli ni kwamba alikuwa ni mtetezi wa wanyonge na alikuwa anapenda kuona haki inatendeka.”
“Pigo ambalo lipo kwenye mioyo ya wengi ni kubwa kwa kweli hakuna anayeweza kuficha hali hiyo, ameondoka wakati bado dunia ikiwa inamuhitaji,” alisema.
Bushoke ni miongoni mwa wasanii ambao wameandika wimbo maalumu kwa ajili ya kumenzi Magufuli, ambaye jana Machi 24 mwili wake uliagwa Mwanza kwa ajili ya wakazi wa mkoa huo kutoa heshima za mwisho kabla ya kupelekwa Chato.