MSANII wa Kizazi Kipya, Beka Flavour amesema watu waliomuibia akaunti za mitandao yake ya kijamii ni watu wake wa karibu wasiomtakia mema.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Flavor alisema hadi sasa akaunti yake ya Instagram imeibiwa mara mbili pamoja na Youtube.
"Mambo haya ambayo sio mazuri, najua nafanyiwa na jamaa zangu, kwa sababu haiwezekani akaunti yangu kama ya Instagram naibiwa mara mbili pamoja na Youtube, sio dalili nzuri, ni wazi wana mpango wakunirudisha nyuma," alisema Flavor.
Beka Flavour aliyetamba na vibao kama ‘Siachani nae’ alidai bado anaendelea kupambana kuona namna anavyoweza kurejesha akaunti zake kwani anaamini ni sehemu ambayo anaitegemea zaidi kujitangaza kibiashara.
Pia Flavor aliwatoa hofu mashabiki wake katika kipindi hiki kigumu anachopitia watulie kwani changamoto sehemu yoyote zipo lakini kikubwa ameanza kujipanga upya kukabiliana na soko la ushindani.