Dar es Salaam. Baraza la Sanaa Taifa nchini Tanzania (Basata) limesema halimtambui Amber Rutty kama msanii na hajasajiliwa na baraza hilo kufanya shughuli za sanaa kama msanii binafsi wala kikundi cha sanaa.
Hayo yameelezwa katika taarifa ya baraza hilo iliyotolewa jana Ijumaa Julai 5, 2019 na kusainiwa na katibu mtendaji wa baraza hilo, Godfrey Mngereza.
Mbali na kumkana Amber, Baraza hilo pia limekemea tabia za baadhi ya watu kuweka picha jongefu kwenye mitandao wakiwa faragha na kuzitaka mamlaka husika zinazosimamia sheria za mitandao kuchukua hatua stahiki kwa wahusika.
“Basata linawakumbusha na kuwaasa wasanii wote kutumia maendeleo ya teknolojia na mitandao ya kijamii kwa lengo la kujiletea maendeleo badala ya kuitumia kusambaza vitu visivyo na manufaa kwao na vyenye kuwadhalilisha wao wenyewe, familia na umma,” inaeleza sehemu ya taarifa hiyo.