Baraza la Sanaa nchini (Basata) limesema linafanyia kazi maagizo ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Harrison Mwakyembe, ya kutakiwa mchukulia hatua msanii Godfrey Tumaini maarufu kwa jina la ‘Dudu Baya’.
Akizungumza leo Jumatano, Februari 26, 2019 na Mwananchi, Ofisa habari wa Basata, Agnes Kimwaga, amesema maagizo hayo wameyapokea na sasa wapo katika kikao ambapo watatoa tamko baadaye kuhusiana na jambo hilo.
Agnes alipoulizwa ni kwani nini siku zote wamekuwa wazito kumchukulia hatua msanii huyo amesema kama Baraza humchukulia msanii hatua kama anakuwa amefanya kosa linalohusisha na sanaa, lakini kwa Dudu Baya kidogo imekuwa ngumu kwani suala lake lilihusisha zaidi makosa ya kimtandao ambayo ni kazi ya Jeshi la Polisi na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).
Hata hivyo, Agnes amesema wanamshukuru Waziri kwa kutoa agizo hilo, ambalo sasa limewapa nguvu ya kumshughulikia Dudu Baya, kwani kama kiongozi mwenye mamlaka anasimamia TCRA na Basata.