Mkali wa sauti, Elius Barnaba ametoa ufafanuzi juu ya kauli yake aliyoitoa hivi karibuni kuwa anamiliki shilingi Bilioni 2.
Barnaba aliweka bayana kuhusu hilo alipokuwa akifanya mahojiano na Wasafi TV mara baada ya kupiga shoo mbili za Bingwa wa Mtaa pande za Mbeya na Morogoro.
“Hii walininukuu vibaya, niliulizwa kwamba ni pesa gani kubwa uliwahi kuishika kwa wakati mmoja ndipo nilisema ni bilioni 2. Niliwahi kushika paap kwa mara moja,” alisema Barnaba.
Akizidi kufafanua kuhusu hilo, Barnaba alisema kiasi hicho cha fedha si kubwa sana hadi watu kuzua gumzo kwani yawezekana kwa sasa anapata nyingi zaidi ya hizo.
“Huwa mimi sio mtu wa kupenda sana kutangaza fedha ninazomiliki lakini kiukweli niliulizwa kiasi kikubwa cha fedha nilichowahi kukimiliki kwa mara moja ndiyo nikasema hiyo,” alisema Barnaba.