Msanii maarufu wa Bongo Fleva ambaye pia ni Official Chawa wa Diamond Platnumz, Baba Levo amefungukia kauli ya Rommy Jones ya kumtaka Mondi aachane na kusaidia wasanii ama watu wa karibu na badala yake ajikite katika kukuza muziki wake.
Baba Levo amedai kuwa, kauli ya Rommy ni chonganishi na ila lengo la kuwanyima ugali machawa wa Diamond kama Baba Levo kwani ndipo sehemu wanapoingizia kipato chao.
Rommy alitoa kauli hiyo kupitia ukurasa wake wa Instagram huku akidai kuwa Mondi amekuwa akisaidia vijana wengi lakini wanapoondoka wanaanza kumsema vibaya na kumdharau ilihali amesaidia kuwa maarufu na kupata pesa nyingi.
“Rommy Jones aache roho mbaya, anaongea kama amechanganyikiwa, sasa tusisaidiwe vipi na Diamond? Acha Diamond atusaidie, tutakaomgeuka tumgeuke ngoma iendelee. Au unataka tufukuzwe?
“Diamond ni mtu wa watu, anatakiwa aishi katika misingi ya kwamba, unapomsaidia mtu usitegemee fadhira, badala yake unamwachia Mungu afungue njia zako, maisha yanaendelea.
“Hawa wanaojitoatoa nao wanatuharibia, mtu umekuja umebebwabebwa, mwisho wa siku unaleta mambo ya hovyo, sio vizuri. Kwa Rommy Jones naona ni roho mbaya imemuingia, ni shetani mbaya. Ewe shetani toka kwa Rommy Jones, toka… toka,” amesema Baba Levo.