Lifestyle

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

SIL

Aliyedhaniwa kufa, arejea nyumbani mazishi yake yakiendelea

56340 Kaburipic Aliyedhaniwa kufa, arejea nyumbani mazishi yake yakiendelea

Sat, 6 Nov 2021 Chanzo: kiswahili.tuko.co.ke

Wakaazi wa Kongelai huko Pokot Magharibi walikula kona kwa hofu na mshtuko wakati mwanamume waliyemdhania kuwa ameaga dunia kuibuka wakati wa kupanga mazishi yake.

Kangrok Muriumeler ambaye ni mfanyabiashara wa mifugo, aliripotiwa kutoweka wiki jana baada ya kuzuru jiji la Nairobi.

Wachuuzi wa mboga katika soko la Konglai walidai mwili uliokuwa ukioza ulitupwa karibu na soko katika eneo hilo na kuwafahamisha maafisa wa polisi waliouchukua.

Wakazi hao walidai baada ya kutambuliwa, familia ilisema mwili huo ulikuwa ni wake Muriumeler na mara moja wakaanza kuandaa mazishi yake.

Mmoja wa wachuuzi wa mboga mboga, Nelly Pusha ambaye alizungumza na The Nairobian alisema aliwafahamisha polisi kuhusu mwili huo ambao ulikuwa umetupwa katika eneo hilo.

"Tulihisi harufu kali kwa siku kadhaa kabla ya kuwafahamisha wakazi wengine na baada ya uchunguzi, tulipata mwili uliokuwa ukioza uliofanana na Muriumeler," alisema.

Mchuuzi huyo alisema jamaa zake walisambaza habari kwamba alitoweka baada ya kupeleka ngombe Nairobi kuuzwa lakini hakurudi tena.

Aliongeza kuwa familia ilipouona mwili huo mara moja walithibitisha kuwa ulikuwa ni wa mpendwa wao na papo hapo maandalizi ya kumzika yakaanza.

Hata hivyo, Muriumeler alisema wenyeji na ndugu zake walidhani alikuwa ameaga dunia na baada ya kufika nyumbani, alishtuka kukuta mipango ya mazishi yake tayari inaendelea.

Alisema alichukua muda mrefu kuwaeleza jamaa zake kuwa bado yu hai, lakini bado hawakuamini.

"Nilikuwa narudi nyumbani kutoka soko la Chepareria nilikutana na watu waliokuwa wakiangalia kiajabu. Waliniambia marafiki na familia yangu walikuwa wakiomboleza kifo changu,” alisema.

“Nilipowasili kutoka Nairobi, sikurudi nyumbani mara moja. Nilifululiza hadi Chepareria kuwaona marafiki zangu na nikalala huko siku mbili.”

Muriumeler alisema kwa mshtuko mkubwa alipokuwa akielekea nyumbani kwake Kongelai, alikutana na waendesha bodaboda ambao walimwambia watu walikuwa wakiomboleza kifo chake.

“Nilikuwa na wakati mgumu kuwathibitishia kwamba nilikuwa hai. Wapo waliokuwa wakiniambia kuwa nimefariki dunia, na kiwiliwili changu kilikuwa kimewatembelea,” alisema huku akitaka kusitishwa kwa mipango ya mazishi mara moja.

OCS wa Kapenguria Lucas Wamocha alisema mwili huo amboa haujulikani ulirudishwa katika makafani ya Hospitali ya Rufaa ya Kaunti ya Kapenguria.

"Mwili bado haujatambuliwa. Haukuwa na majeraha popote. Inaonekana marehemu aliuawa kwingine na kutupwa. Tumesambaza taarifa hizo kwenye mtandao wetu wa polisi, lakini hatujapata taarifa za watu waliopotea,” alisema.

Chanzo: kiswahili.tuko.co.ke