Dar es Salaam. Mbunge wa Starehe nchini Kenya, Charles Njagua maarufu Jaguar amesema anaipenda Tanzania na upendo huo wanauonyesha hata katika kazi zake za muziki.
Jaguar amesema hayo leo Ijumaa Julai 19,2019 alipokuwa akizungumza na Mwananchi kwa simu akiwa Dar es Salaam nchini Tanzania.
Msanii huyo ambaye siku za hivi karibuni alitoa kauli iliyoibua mjadala mkali hadi viongozi wa juu, Rais John Magufuli na Uhuru Kenyatta wa Kenya walipoizungumzia na kuwasihi wananchi wa mataifa hayo kuwa watulivu na wasikubali kugombanishwa.
Katika mahojiano yake na Mwananchi, Jaguar amesema, “Nawapenda sana Watanzania.”
“Mimi Tanzania nina kijana (mtoto) nimekuja kumwona, ndio maana ninawapenda Watanzania na ninawapenda warembo (aki maanisha wanawake) wa Tanzania,” amesema Jaguar
Mwananchi lilipotaka kujua mara baada ya kuwasili Tanzania, hajakutana na changamoto yoyote, Jaguar amesema, “ilikuwa poa tu hakuna tatizo kabisa na Watanzania wananipenda.”
Habari zinazohusiana na hii
“Hata kimziki, Tanzania wananiunga mkono sana na yale walichukulia misemo yangu vibaya, Watanzania ilikuwa kwa wachina,” amesema
Kuhusu kufanya tamasha Tanzania, Jaguar amesema, “Kwa sasa nawakilisha jimbo la starehe kwanza.”
Juni 25, 2019 mbunge huyo kupitia mitandao ya kijamii video yake ilisambaa akieleza kuwafukuza wafanyabiashara wa kigeni wakiwemo Watanzania ndani ya masaa 24 kurudi kwao la sivyo watawapiga na kuwarudisha nchini mwao.
Serikali ya Kenya ililaani kauli yake hiyo na kusema si msimamo wa nchi hiyo, pia alikamatwa na kusota rumande kwa siku nne katika kituo cha Polisi Kileleshwa baada ya mahakama kusema kuna haja ya kulinda uchunguzi unaoendeshwa kuhusu matamshi ya uchochezi anayodaiwa kuyatoa. Hata hivyo aliachiwa kwa dhamana.