BAADA ya kukaa chumba cha majeruhi kwa mwezi mzima akiuguza jeraha la goti, mshambuliaji wa JKT Tanzania, Adam Adam, amesema kwa sasa anaendelea vizuri na yupo fiti kurejea dimani pindi ligi hiyo itakapoendelea tena.
Akizungumza na Nipashe jana, Adam alisema kwa sasa anashukuru hali yake imeimarika na tofauti na mwanzo.
"Nashukuru, naendelea vizuri na ninafanya mazoezi ili kuuweka sawa mwili wangu kujiandaa na ligi," alisema Adam ambaye hadi anapata majeraha hayo, alishatupia mabao sita kwenye Ligi Kuu.
Aidha, aliwashukuru wachezaji wenzake pamoja na uongozi kutokana na ushirikiano waliompa siku zote akiwa anauguza majeraha hayo.
"Naushukuru uongozi wangu walinisaidia na kunijali kipindi chote ambacho nilikuwa mgonjwa mpaka sasa," alisema.