Mwanamke mwenye umri wa miaka 28 na mumewe wenye uraia wa Brazil na Uhispania wanadaiwa kuvamiwa na kujeruhiwa vibaya huku mwanamke huyo akidai kubakwa na wanaume 7, Tukio hilo limetokea wakati wakiwa katika ziara ya pikipiki nchini India baada ya kusimama usiku katika wilaya ya Dumki wakati shambulio hilo linalodaiwa kutokea.
Polisi wanasema wamewakamata wanaume wanne na wanawasaka wengine watatu.Vitambulisho vya wanaume hao ambao pia wanadaiwa kumpiga mpenzi wa mwanamke huyo bado havijawekwa wazi.
Wenzi hao walikuwa wamesafiri sehemu kadhaa za Asia kwa pikipiki zao kabla ya kuwasili India miezi michache iliyopita.
"Wanaume saba walinibaka. Wametupiga na kutuibia, ingawa si vitu vingi wamechukua kwa sababu walichotaka ni kunibaka," alisema kwa lugha ya Kihispaniola na kuongeza kuwa wanaume hao waliwapiga na kutishia kuwaua.
Katika video nyingine tofauti, mume huyo ambaye ni Mhispania alisema “Mdomo wangu umeharibika kwa kipigo, lakini mwenzangu amefanyiwa ukatili mbaya kuliko mimi."
Msimamizi wa polisi wa Dumka, Pitamber Singh Kherwar alisema, "Wanandoa hao walikuwa wakizungumza kwa mchanganyiko wa Kiingereza na Kihispania hivyo timu ya doria haikuweza kuwaelewa mwanzoni. Lakini walionekana kujeruhiwa waziwazi hivyo walipelekwa hospitalini kwa matibabu," alisema na kuongeza kwamba wanandoa hao waliwaambia madaktari kuhusu madai ya ubakaji.
Tuhuma hizo za ubakaji kwa mtalii huyo mwenye uraia wa Brazil na Uhispania katika jimbo la mashariki mwa India la Jharkhand limeibua hisia na watu wengi kukasirishwa na kitendo hicho.