Dar es Salaam. Raia wa Afrika kusini, Abaasi Suguya na mkazi wa Vingunguti, Fon Kabwe wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na shtaka la kusafirisha dawa za kulevya aina ya heroin zenye uzito wa gramu 501.11.
Akisoma hati ya mashtaka leo Alhamisi Mei 9, 2019 mbele ya Hakimu Mkazi, Janeth Mtega, wakili wa Serikali, Faraji Nguka amedai washtakiwa hao wanakabiliwa na kosa la uhujumu uchumi la kusafirisha dawa za kulevya kinyume na sheria.
Nguka amedai Septemba 20, 2019 maeneo ya stendi ya mabasi ya Ubungo, washtakiwa hao walisafirisha dawa hizo huku wakijua kufanya hivyo ni kosa.
Amedai upelelezi bado haujakamilika na kuomba mahakama hiyo ipange tarehe nyingine.
Baada ya kusomewa mashtaka hayo hakimu Mtega amesema washtakiwa hawakutakiwa kujibu chochote kwa kuwa mahakama hiyo haina uwezo wa kusikiliza kesi hiyo.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Mei 23, 2019 na washtakiwa kurudishwa rumande kwa kuwa shauri lao halina dhamana.