Geita. Watumishi watatu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoani Geita wanashikiliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kwa mahojiano kwa tuhuma za kuwafanyia makadirio ya juu wafanyabiashara na badaye kuwashawishi kutoa rushwa ili wawakadirie kadirio la chini.
Kaimu Ofisa Takukuru mkoa wa Geita, Mwamba Masanja akizungumza na Mwananchi leo Jumanne Juni 18,2019 amewataja wanaoshikiliwa ni Sadick Lutenge, Amza Rugemalira na Elias Msula
Amesema watuhumiwa hao wanadaiwa kutenda makosa hayo kinyume na kifungu cha 15(1) (a na b) na (2) cha sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa namba 11 ya mwaka 2007.
Miongoni mwa tuhuma zinazochunguzwa na Takukuru ni maofisa hao kuomba rushwa zaidi ya Sh100 milioni kutoka kwa wafanyabiashara watatu tofauti kwa kipindi cha Aprili na Juni mwaka 2019.
Kukamatwa kwa watuhumiwa hao kumekuja siku chache baada ya Rais wa Tanzania, John Magufuli kukutana na wafanyabiashara na kuelezwa changamoto zao ambapo miongoni mwa changamoto walizozieleza ni kukadiriwa kodi kubwa na maofisa wa TRA.