Watu watano wamefariki dunia wakati wakikimbizwa hospitalini baada ya kujeruhiwa katika piga nikupige na Jeshi la Polisi usiku wa kuamkia jana.
Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa jana na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Awadhi Haji, waliouawa wanakadiriwa kuwa na umri kati ya miaka 20 hadi 30.
Aidha, alisema tukio hilo limetokea saa 7:30 katika
Kitongoji cha Nyangozi Kijiji cha Mugera Kata ya Nyantakara, Tarafa ya Lusahunga wilayani Biharamulo.
“Majira ya saa tano usiku askari walipata taarifa kutoka kwa raia wema kuwa katika Pori la Hifadhi ya Msitu wa Biharamulo kuna kikundi cha watu ambao idadi yao inakadiriwa kuwa tisa wakiwa wamejificha kwenye pori hilo na wamepanga kuwateka wafanyabiashara watakaoenda kwenye soko la Nyakanazi la jana.”
Alisema, askari baada ya kupata taarifa hiyo walijipanga na kuanza ufuatiliaji kwa kutumia askari wa
kikosi cha kupambana na majambazi walioelekea eneo la maficho katika pori hilo mahali walipodaiwa kuwepo watu hao.
Alisema askari hao walipofika hapo walirushiwa risasi na majambazi hao na ndipo na wao walipojibu na kufanikiwa kuwajeruhi majambazi watano katika eneo la tukio lakini walikufa wakikimbizwa hospitalini kwa matibabu.
Alisema polisi imefanikiwa kukamata bunduki mbili aina ya Ak-47 zilizofutika namba, bunduki nyingine mbili zenye risasi 27 na bomu moja la kutupa kwa mkono.