Jeshi la Polisi mkoa wa Mbeya, linawashikilia watu 45 kwa tuhuma za makosa mbalimbali ikiwemo watu 12 kuhusika na mauaji katika kipindi cha kuanzia Desemba mosi mpaka 23 mwaka huu
Kamishna Msaidizi wa Polisi, mkoa wa Mbeya ACP Benjaman Kuzaga, amethibitisha hayo alipozungumza na wanahabari kuhusu mafanikio ya Jeshi hilo katika kipindi cha mwezi Desemba
Amesema kati ya watuhumiwa 12 wa mauaji tayari watano wamefikishwa mahakamani kwa ajali ya hatua za kisheria na wengine saba upelelezi unaendelea
Ameongeza kuwa Jeshi hilo limefanikiwa kuwakamata watu wawili kwa tuhuma za kupatikana na silaha aina ya Gobole ikiwa na risasi 50 pamoja na fataki 32 wilayani Chunya
“Haya ni miongoni mwa mafanikio ya Jeshi Polisi katika kipindi cha Desemba mosi mpaka 23 ambapo kupitia doria na misako mbalimbali tulifanikiwa kuwakamata watuhumiwa 45 kwa makosa ya kupatikana na silaha bila kibali, dawa za kulevya, kuingiza bidhaa zilizopigwa marufuku, mauaji pamoja na nyara za Serikali,”amesema Kuzaga
Ameongeza kuwa Jeshi la Polisi limeandaa utaratibu wa kupima kiwango cha ulevi kwa madereva wote wa Mkoa huo, lengo ni kukabiliana na ajali za barabarani msimu wa sikukuu za mwisho wa mwaka
Amesema tayari Polisi wametawanyika kwenye vizuizi mbalimbali mkoani Mbeya ili kupima watu na watakaobainika watachukuliwa hatua za kisheria.