Tunduru. Polisi wilayani Tunduru, Mkoa wa Ruvuma inawashikilia watu 45 wakihusishwa na ulanguzi wa korosho zaidi ya tani 17 za thamani ya Sh56.1 milioni ambazo zimetaifishwa na Serikali.
Akizungumza na Mwananchi leo, Jumanne Novemba 13, 2018, Mkuu wa Wilaya ya Tunduru, Juma Homera amesema watu hao wamekamatwa kwenye operesheni maalumu inayoendelea ya kamata walanguzi wanaowalaghai wakulima na kununua korosho kwa mfumo usio rasmi maarufu ‘kangomba’.
Amesema walanguzi hao huwarubuni wakulima kwa kununa korosho zao kwa Sh1,000 kwa kilo moja.
Homera amesema Serikali ipo macho na itahakikisha inawachukulia hatua wafanyabiashara wote ambao wanajihusisha na biashara hiyo kwani haiko tayari kuona wananchi wakionewa.
Jana, Jumatatu Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Christina Mndeme alifanya ziara ya ghafla wilayani humo na kutaifisha tani 11 za korosho ambapo watu 39 walikuwa wakishikiliwa.
Usiku wa kuamkia leo, Jumatano, idadi ya watuhumiwa imeongezeka na kufikia 45 na tani zimeongezeka na kufikia 17 baada ya sita kukamatwa usiku zikiwa na watuhumiwa sita akiwemo mwalimu.
Soma zaidi:
Maagizo mazito ya Magufuli
Zitto aupokea uamuzi wa Serikali kununua korosho lakini...