Wachimbaji wadogo wa Madini wapatao 16 wa Mererani Mkoani Manyara, wanashikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani humo kwa tuhuma za kukutwa na gramu 700 za madini ya Tanzanite wakiwa kwenye kitalu C kinachomilikiwa na Serikali
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Manyara, Kamishna Msaidizi Mwandamizi, Marison Mwakyoma alithibitisha kukamatwa kwa watuhumiwa hao wakiwa kwenye kitalu hicho.
Aidha,alisema kuwa bado hawajapata taarifa kamili ya thamani ya madini hayo waliyoyakamata kwani wanasubiria ripoti yaTume ya Madini Tanzania, hivyo watuhumiwa hao bado wanaendelea kuhojiwa na jeshi hilo kabla ya kufikishwa Mahakamani kwa ajili ya kujibu mashtaka yanayowakabili.
“Natoa wito kwa wachimbaji kutojihusisha na kuingia bila halali kwenye kitalu C, ambacho ni mali ya serikali kwani tutaendelea kuwachukulia hatua kali”.
kamanda huyo alitoa rai kwa wananchi kushirikiana na Jeshi la polisi kwa kutoa taarifa punde wanapobaini uhalifu ili kudumisha amani na usalama wa nchi.