Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoani Mara imeshinda kesi dhidi ya Wibiro Chacha Makuru, Tabani Banosi Matoro na Chacha Mwita Bwiri ambao walishitakiwa kwa makosa matano ya rushwa.
Hukumu hiyo iliyotolewa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Serengeti, Ismail Ngaile ilitokana na Kesi ya Jinai Namba 320 iliyofunguliwa Mwaka 2018 na kuendeshwa na Wakili William Lyamboko.
Awali ilielezwa na Lyamboko mahakamani hapo kuwa, Mshtakiwa wa Kwanza ni Makuru (Kaimu Mwenyekiti wa Kijiji cha Kenyana), wa Pili ni Matoro (Mwenyekiti wa Kitongoji cha Mokehogo) na wa Tatu ni Bwiri (Katibu wa Kamati ya Ardhi ya Kijiji cha Kenyana).
Wote wamepatikana na hatia kwa makosa yote matano na wamehukumiwa kifungo cha jela kwa miaka mitano kila mmoja.
Hata hivyo wakati hukumu hiyo ikitolewa, Makuru hakuwapo mahakamani hivyo Ngaile alitoa kibali cha kumtafuta na kumkamata ili akatumikie adhabu yake gerezani.