Mtwara. Watu watano wamefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Newala mkoani Mtwara nchini Tanzania kwa tuhuma za kukamatwa na dawa za kulevya aina ya heroin kilo saba na gram tisa katika maeneo tofauti wilayani Newala kufuatia operesheni ya kikosi kazi cha Taifa Operesheni Kambale wakiwa doria.
Pia, wenzao watano wanaendelea kushikiliwa mpaka taratibu za kimashtaka zitakapokamilika na kisha kupeleka mkoani Mtwara kuunganishwa na wenzao.
Akizungumza na waandishi wa habari mkoani Mtwara jana Ijumaa Julai 5, 2019, Mkuu wa Operesheni maalum za Jeshi la Polisi, Mihayo Msikhela alisema Juni 10, 2019 majira ya saa 9:30 kikosi hicho katika kijiji cha Chihanga Newala walimkata mtuhumiwa wa kwanza, Rajab Mchingama akiwa anasafirisha vifurushi nane vya dawa za kulevya kwa kutumia pikipiki.
Alisema siku hiyohiyo majira ya saa 11 jioni walimkamata mtuhumiwa mwingine, Salum Mtili mkulima na mkatishaji wa tiketi za abiria wanaokwenda Msumbiji na siku iliyofuata walimkamata mtuhumiwa Jeremiah Mulenga mkazi wa Magomeni jijini Dar es Salaam akiwa wilayani Masasi mkoani Mtwara.
“Ufuatiliaji uliendelea kwa timu kuelekea Dar es Salaam kuendelea na mnyororo wa ukamataji na majira ya saa 10 eneo la Magomeni Mapipa askari walifanikiwa kumkamata Kelvin Mgosi na ili kutoweza kuupata mtandao wote aliwasiliana na mwenzake na kushawishi rushwa kwa askari,” alisema Msikhele
Alisema katika mtego uliowekwa walimnasa Jeremiah Mulenga akiwa na Sh1.1 milioni alizotumwa kwenda kuwakomboa wenzao waliokuwa chini ya ulinzi na kwamba waliendelea kuutaja mtandao wao wa waagizaji, wasambazaji na wauzaji wa dawa za kulevya toka nchi jirani ambao wanaendelea kuufuatilia.
Pia Soma
- Mume aangua kilio mahakamani akielezea jinsi mke wake alivyouawa
- Waziri wa Misri aahidi ushirikiano ujenzi mradi wa umeme Rufiji
- Majaliwa aongoza harambee ya kuchangia ujenzi wa kitega uchumi CCT