Kikosi maalum cha askari wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori (Tawa ) Kanda ya Kaskazini kimeanza msako katika vijiji vinavyozunguka eneo la mapito ya wanyamapori la Mswakini lililopo mpakani mwa mkoa wa Manyara na Arusha kubaini waliohusika kuua simba watatu.
Akizungumza na leo Jumanne Machi 29, 2022 Kaimu Kamanda wa Uhifadhi wa Tawa Kanda ya Kaskazini, Peter Mbanjoko amesema simba hao wameuawa na kutolewa baadhi ya viungo na watu wanaodaiwa kujeruhiwa na simba hao.
"Tumepata taarifa za kuuawa simba hao na watu ambao wamejeruhiwa na simba hao kabla ya kuwaua, watu hao wamejificha hivyo askari wapo eneo la tukio kuwatafuta waliohusika na mauaji hayo kwani ni kinyume cha sheria.
"Hakuna sababu yoyote ya kuua simba, huu ni ujangili na tunawasaka watuhumiwa na wakipatikana watafikishwa kwenye vyombo vya sheria"amesema