WAHAMIAJI haramu 22 wamefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Mpanda mkoani Katavi kwa makosa ya kuingia na kuishi nchini bila kuwa na vibali halali.
Waliofikishwa mahakamani ni raia 18 wa Burundi na raia wanne ambao ni raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).
Hao ni miongoni mwa wahamiaji haramu 40 waliokamatwa hivi karibu na maofisa wa idara ya uhamiaji katika Mkoa wa Katavi.
Kamanda wa Uhamiaji Mkoa wa Katavi, Vicent Haule alisema hayo alipozungumza na wanahabari juzi mjini hapa.
Alieleza kuwa miongoni mwao, raia kutoka Burundi ni 18, DRC wanne na 12 uraia wao haujafahamika na wanaendelea kuchunguzwa.
"Wahamiaji haramu sita wakiwemo watano kutoka Burundi na mmoja raia wa DRC watarejeshwa nchini mwao," alieleza
Alisema wahamiaji hao haramu, walikamatwa na maofisa uhamiaji katika msako uliofanyika vijiji vya Ikola, Kabungu, Magamba, Mparamawe na Majalila.