Babati. Jeshi la polisi Mkoani Manyara linawashikilia watu wanne kwa tuhuma za kumuua kwa kumkata mapanga mkazi wa Kijiji cha Bashang' wilayani Hanang.
Akizungumza na Mwananchi leo Ijumaa Desemba 28, 2018 kamanda wa polisi wa mkoa wa Manyara, Augustino Senga amemtaja mtu aliyeuawa kuwa ni mkulima wa kijiji hicho, Malendi Gidamashuku (50).
Kamanda Senga amesema chanzo cha kifo hicho bado hakijajulikana ila polisi wanaendelea na uchunguzi wa tukio hilo.
"Watu hao tunawashikilia wakidaiwa kumuua mwanakijiji mwenzao baada ya kumkatakata kwa mapanga sehemu mbalimbali za mwili wake," amesema kamanda Senga.
Amewataja watu hao wanashikiliwa na polisi ni Naweda Kipara (29), Regina Gidawang (21), Paschal Andrew (24) na Phabiano Giam (20) ambao ni wakazi wa kijiji cha Bashang'.
Amesema wanaendelea na uchunguzi wa tukio hilo kabla ya kuwafikisha mahakamani wakajibu mashtaka yanayowakabili.