T: Wanne kortini kwa kukutwa na nyama ya kibok
Dar es Salaam. Watu wanne wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashtaka mawili likiwemo la kukutwa na kilo 200 ya nyama ya kiboko yenye thamani ya Sh3.44milioni.
Washtakiwa hao ni Ayoub Kayanda, Jumanne Sia, Said Lwambo na Ally Nongu.
Akisoma hati ya mashtaka leo Jumatano Mei 29, 2019 mbele ya hakimu mkazi mwandamizi, Augustine Rwizile, wakili wa Serikali, Sada Mohamed amedai washtakiwa hao wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi namba 44 ya mwaka 2019.
Amedai katika kosa la kwanza la kukutwa na nyara za serikali kwa pamoja wanadaiwa Mei 9, 2019 wakiwa Nzasa Wilaya ya Temeke walikutwa na kilo hizo huku wakiwa hawana kibali cha mkurugenzi wa wanyamapori.
Katika shtaka la pili la kujihusisha na nyara za Serikali wanadaiwa kwa pamoja kati ya Mei 7 na 9, 2019 katika maeneo tofauti jijini Dar es Salaam na Mkoa wa Pwani walikubali kusafirisha kilo 200 za nyama ya kiboko.
Pia Soma
- Kiongozi mbio za mwenge awapa somo watumishi wa umma
- Ilichokisema NEMC kuhusu mifuko ya plastiki
- Fundi nguo asimulia alivyotekwa, adai kuibiwa Sh5milioni
Hakimu Rwizile amesema washtakiwa hawaruhusiwi kujibu chochote baada ya kuibuka hoja kama mahakama hiyo inapaswa kusikiliza kesi hiyo ama la.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Mei 31, 2019 na washtakiwa kurudishwa rumande.