Wafanyabiashara watatu, Goodness Remy mkazi wa Salasala, Emmanuel Chigbo Mkazi wa Goba na Paulina Mwanga mkazi wa Kibaha wamefikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na Mashtaka ya Uhujumu Uchumi na kusafirisha kilo 58.62 za dawa za kulevya aina ya Heroin.
Wakili wa Serikali, Frank Michael, ameiambia Mahakama kuwa, washtakiwa walitenda kosa hilo Aprili 19, 2023 eneo la Salasala, Kinondoni jijini Dar es Salaam ambapo walikutwa na Dawa aina ya Heroin.
Upande wa Jamhuri uliomba Mahakama kupanga tarehe nyingine kwasababu upelelezi haujakamilika. Kesi imeahirishwa hadi Juni 1, 2023 na washtakiwa wote wamerudishwa Mahabusu kwa kuwa kesi yao haina dhamana.