JESHI la Polisi mkoa wa Pwani limewafikisha mahakamani watu wanane kwa tuhuma za kukutwa na meno ya tembo yenye uzito wa kilogramu mbili yakiwa na thamani ya Sh milioni tano na bunduki sita aina ya gobori.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Pwani, Wankyo Nyigesa aliwaambia waandishi wa habari juzi kuwa, hayo ni mafanikio ya misako na operesheni zilizofanyika kuanzia Septemba Mosi hadi 30, mwaka huu mkoani humo.
Alisema watu hao walikutwa na vitu hivyo katika nyumba ya mmoja watuhumiwa hao iliyopo Chalinze wilaya ya Bagamoyo na wamefikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazokabili.
Alisema operesheni hizo zimesaidia kukamata watu 95 ambao kati yao, wanaume 69 na wanawake 26 na watuhumiwa 64 wamefikishwa mahakamani kwa tuhuma mbalimbali.
"Katika operesheni hiyo na misako iliyoendeshwa kwenye bandari bubu ili kudhibiti wafanyabiashara wanaotumia bandari bubu hizo kupitisha bidhaa zisizolipiwa ushuru, jumla ya watu sita wamekamatwa na kuokoa mafuta ya kula ya aina mbalimbali lita 3,440 na dizeli lita 40," alisema Nyigesa.
Aliwataka wananchi kufanya shughuli halali na kuacha kutaka kipato kwa njia zisizo halali kwani endapo watajihusisha na vitendo vya kihalifu hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.