Dar es Salaam. Zheng Rongman na mkewe, Ou Ya wote raia wa China wamefikishwa katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwa tuhuma za kutoa rushwa ya Dola 5,000 za Kimarekani sawa na Sh11.5 milioni kwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato nchini Tanzania (TRA), Dk Edwin Mhede.
Rongman ambaye ni mkurugenzi mtendaji wa kampuni ya Ronglan Intl Industry and Trade Co Ltd na mkewe wamekiri kutaka kutoa rushwa kwa bosi huyo wa TRA. Wanandoa hao ni wakazi wa Wilaya ya Mafinga mkoani Iringa.
Wamefikishwa mahakamani leo Jumanne Februari 25, 2020 na kusomewa shtaka moja la kutoa rushwa.
Akiwasomewa hati ya mashtaka wakili wa Takukuru, Ipyana Mwakatobe amedai mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi kuwa washtakiwa wanakabiliwa na kesi ya jinai namba 30/2020.
Mwakatobe amesema washtakiwa wanadaiwa kutenda kosa hilo Februari 24, 2020 makao makuu ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), jijini Dar es Salaam.
Imedaiwa kuwa siku ya tukio walitoa rushwa kwa Dk Mhede ili kumshawishi iwasaidie kampuni yao isilipe kodi ya Sh1.3 bilioni.
Pia Soma
- Wanafunzi bora Kisarawe kuzawadiwa vifaa vya umeme
- VIDEO: Alichosema Dk Mashinji baada ya Mdee kukataa salamu yake
- Bashiru awashukia wenye ajenda ya tume huru 2020
Hakimu Shaidi amesema kesi hiyo itaendelea kesho kwa ajili ya kusomewa maelezo ya awali.
Pia Hakimu Shaidi ameutaka upande wa mashtaka kumleta mkalimani kwa ajili ya mshtakiwa wa kwanza ambaye hajui vizuri lugha ya Kiingereza.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Februari 26, 2020 itakapoendelea na washtakiwa wamerudishwa rumande.