Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Wanandoa na 'hausiboi' kortini wakidaiwa kusafirisha dawa za kulevya

Madawa Kusafirisha Kisutu.png Wanandoa na 'hausiboi' kortini wakidaiwa kusafirisha dawa za kulevya

Fri, 29 Dec 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Wanandoa pamoja na mfanyakazi wao wa ndani wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam wakikabiliwa na mashtaka ya kusafirisha dawa za kulevya aina ya heroine na methamphetamine zenye uzito wa kilo 3,050.

Wanandoa hao ni Najim Mohamed (52) ambaye ni mfanyabiashara na mkewe Maryam Mohamed (51), wakazi wa Kigamboni-Kibugumo pamoja na mfanyakazi wao wa ndani, Juma Abbas (37).

Washtakiwa hao wamefikishwa mahakamani hapo leo, Desemba 29, 2023 na kusomewa mashtaka ya uhujumu uchumi katika kesi namba 53/2023 na Wakili Mwandamizi wa Serikali, Hemed Halfan akishirikiana na Frank Michael mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi, Aaron Lyamuya.

Mshtakiwa Najim Mohamed(52) akiwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, akikabiliwa na mashtaka na mashtaka ya kusarisha dawa za kulevya. Picha na Hadija Jumanne

Hata hivyo, kabla ya kusomewa mashtaka yao, Hakimu Lyamuya amesema washtakiwa hawatakiwi kujibu chochote kwa kuwa mahakama hiyo haina uwezo wa kusikiliza kesi za uhujumu uchumi, isipokuwa Mahakama Kuu ndio yenye uwezo wa kusikiliza shauri hilo.

Akiwasomea mashtaka hayo, Wakili Halfan alidai Desemba 15, 2023 eneo la Kibugumo Shule lililopo Wilaya ya Kigamboni, washtakiwa kwa pamoja walisafirisha dawa za kulevya aina ya heroine zenye uzito wa kilo 882.71.

Katika shtaka la pili, wanadaiwa siku na eneo hilo, walisafirisha dawa za kulevya aina ya methamphetamine zenye uzito wa kilo 2167.29.

Upande wa mashtaka ulidai upelelezi haujakamilika, hivyo kuomba tarehe nyingine ya kutajwa.

Hakimu Lyamuya alikubali ombi la upande wa mashtaka na kuahirisha kesi hadi Januari 11, 2024 itakapotajwa.

Hakimu Lyamuya amesema mashtaka yanayowakabili washtakiwa hao hayana dhamana kwa mujibu wa sheria, hivyo wataendelea kubaki rumande.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live