Serengeti. Washtakiwa wanne waliokamatwa na nyama ya pundamilia kila mmoja amehukumiwa kifungo cha miaka 20 jela na Mahakama ya Hakimu mkazi mfawidhi wilaya ya Serengeti.
Katika kesi hiyo ya uhujumu uchumi namba 55/2018, Hakimu Ismael Ngaile amewahukumu kila mmoja kwenda jela miaka 20.
James Mwita na Yohana Mahende wakazi wa Kisangura walikutwa na nyama hiyo yenye thamani ya Sh2,616,000 huku Athumani Zakaria na Juma Chacha wakazi wa kijiji cha Bisarara walikutwa na miguu ya mnyamapori huyo.
Leo Ijumaa Julai 26, 2019 waendesha mashitaka Elisa Benjamin na Emmanuel Zumba wameiambia mahakama hiyo kuwa washtakiwa walikamatwa katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti mwaka 2018.