Mbunge wa Kisesa, Luhwaga Mpina amepinga majibu ya Serikali kuhusu kauli kuwa hawana taarifa ya agizo la Mahakama kuhusu kurudisha mifugo ya wafugaji kama ilivyoamuliwa na mahakama.
Mpina amesema inashangaza na kusikitisha kuona kuwa, Mahakama ilishamuru wafugaji warudishiwe mifugo yao ambayo ilikuwa imeporwa na watu wa TFS, TAWA na WMA na kwamba jambo hilo lilishazungumzwa na kutolea agizo na Waziri Mkuu.
“Hii inashangaza sana kuona leo Serikali inakataa kuwa haina taarifa hizo kuhusu mifugo, nataka kujua ni lini hasa wafugaji hawa watarudishiwa mifugo yao kama mahakama ilivyoagiza,” amehoji Mpina.
Haata hivyo katika majibu yake Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja amesema kuwa Wizara yake haina taarifa kuhusu agizo hilo kwamba wafugaji wapewe mifugo yao.
Masanja amesema kazi ya Serikali katika kesi hizo ni kupeleka vielelezo tu na hivyo wanaamini kuwa kila kitu kitatolewa ikiwa tu Wizara itapata taarifa sahihi ya nini kinatakiwa.
Amewataka wafugaji wanaodai mifugo yao kufanya mawasiliano na Wizara hiyo mapema iwezekanavyo na wakipokea taarifa hiyo watakaa pamoja kuchambua kesi hizo ili kuwalipa au kuwarudishia fidia wafugaji hao.
Advertisement