Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Walimu kortini kwa kufanya kazi bila vibali

Tue, 14 May 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Walimu wanne akiwemo meneja wa Shule ya Msingi na Sekondari Kings, Stella Shuma wamefikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashtaka mawili likiwemo la kufanya kazi nchini bila ya kuwa na kibali cha Idara ya Uhamiaji.

Mbali na Stella wengine ni raia wa Kenya, Ezron Maina, Ruth Frank, Joseph Kuria na Charles Sakawa.

Wakili wa Serikali, Faraji Nguka akisoma hati ya mashtaka mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Augustine Rwezile, alidai kuwa   washitakiwa walitenda makosa hayo kati ya Septemba, 2018 na Machi, 2019 eneo la Goba, Wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.

Ilidaiwa kwamba katika shtaka la kwanza, Maina, Ruth, Kuria na Sakawa katika kipindi hicho, jijini Dar es Salaam, walikutwa wakifanya kazi katika shule hiyo wakati wakijua hawana kibali kutoka Idara ya Uhamiaji.

Shitaka la pili linalomkabili Stella anayedaiwa kwamba katika kipindi na eneo lilipofanyika kosa la kwanza akiwa meneja wa Shule ya Kings aliwaajiri washitakiwa hao huku akijua ni raia wa Kenya na hawana kibali kutoka Idara ya Uhamiaji.

Washitakiwa wote walikana makosa hayo na waliachiwa kwa dhamana baada ya kutimiza sharti la kuwa na mdhamini mmoja aliyesaini bondi ya Sh5 milioni pamoja na washitakiwa hao kujidhamini wenyewe kwa kiasi hicho cha fedha.

Pia Soma

Kesi hiyo iliahirishwa hadi Mei, 15 mwaka huu itakapotajwa tena huku upelelezi ukiwa haujakamilika.

Chanzo: mwananchi.co.tz