Jeshi la Polisi mkoani Mbeya, limewakamata Watuhumiwa watano kwa kosa la kuiba na kufanyia uhalifu bastola ikiwa na risasi 11, ambapo baadaye Polisi walibaini kuwa bastola hiyo ni mali ya Mkuu wa Wilaya ya Sikonge, John Palingo.
Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya, Ulrich Matei amesema Wahalifu hao wamekutwa na Mali nyingine za wizi lakini hajaweka wazi mazingira yaliyopelekea bastola ya DC kukutwa mikononi kwa Wahalifu.
Katika hatua nyingine kamanda Matei amesema jeshi la polisi limepata taarifa za kiintelijensia kuhusu watu wanaojipanga kufanya maandamo jijini Mbeya, na kutoa onyo kali kwa watu hao.
Kamanda Matei ametoa wito kwa wananchi mkoani Mbeya kutoa taarifa za uhalifu na wahalifu ili hatua ziweze kuchukuliwa na kuhakikisha watu wanaishi kwa amani na utulivu.