Dar es Salaam. Upelelezi wa kesi inayomkabili mshereheshaji maarufu nchini, Anthony Luvanda ‘MC Luvanda’ bado haujakamilika, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeelezwa leo Jumatatu Januari 21, 2019.
Wakili wa Serikali, Elizabeth Mkunde amedai leo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama hiyo, Huruma Shaidi kuwa upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika hivyo wanaomba tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa.
Mkunde baada ya kueleza hayo, wakili wa utetezi, Jebra Kambole ameutaka upande wa mashtaka kuhakikisha kuwa wanakamilisha upelelezi wao kwa wakati ili kesi hiyo iweze kuendelea.
Mbali na Luvanda, mshtakiwa mwingine katika kesi hiyo ni kampuni ya Luvanda ya Home of Company Limited,
MC Luvanda na kampuni yake wanakabiliwa na mashtaka matatu likiwemo la kutumia kikoa ambacho hakijasajiliwa Tanzania pamoja na kutoa maudhui mtandaoni bila kuwa na kibali cha Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).
Mshtakiwa huyo alifikishwa kwa mara ya kwanza katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Septemba 24, 2018 kujibu mashtaka yanayomkabili.
Hakimu Shaidi baada ya kusikiliza hoja za pande zote, ameahirisha kesi hiyo hadi Februari 20, 2019 itakapotajwa na mshtakiwa yupo nje kwa dhamana.
Inadaiwa kuwa kati ya Februari 24 na Septemba 2018 katika Jiji la Dar es Salaam, mshtakiwa alianzisha na kutumia mtandao wa www.mcluvanda.com ambao haukuwa na kikoa cha .tz.
Pia inadaiwa kuwa katika kipindi hicho mshtakiwa alianzisha na kutumia mtandao huo ambao haukuwa na kikoa cha .tz.
Katika shtaka la tatu, mshtakiwa anadaiwa kutoa huduma ya online bila ya kuwa na kibali.
Anadaiwa katika kipindi hicho alitoa huduma hiyo kupitia online TV ijulikanayo kama MC Luvanda bila kibali cha TCRA.
Soma Zaidi: Upelelezi kesi ya MC Luvanda wasubiri taarifa za Brela