Dar es Salaam. Upande wa mashtaka katika kesi ya utakatishaji fedha inayomkabili aliyekuwa meneja wa Benki ya Wanawake Tanzania (TWB) tawi la Mkwepu, Priscus Shirima umedai mshtakiwa huyo yupo kwenye hatua ya mwisho za makubaliano kwa kuwa amekiri makosa yanayomkabili.
Akizungumza leo Jumatatu Oktoba 7, 2019 wakili wa Serikali mwandamizi, Wankyo Simon amedai mshtakiwa amekiri na kuomba msamaha hivyo yupo kwenye hatua ya mwisho kwa ajili ya makubaliano.
"Mheshimiwa naiomba mahakama hii ipamge tarehe nyingine kwa kuwa wakili wa mshtakiwa yupo kwenye makubaliano hivyo naomba tarehe ya kesho," amedai Simon.
Hakimu Mfawidhi wa mahakama hiyo, Kelvin Mhina ameiahirisha shauri hilo hadi Oktoba 8,2019.
Shirima alifikishwa kwa mara ya kwanza katika Mahakama ya Kisutu Desemba 13, 2018 kujibu mashtaka hayo.
Kwa mujibu wa hati ya mashtaka, mshtakiwa anadaiwa kufanya muamala wa uongo akiwa ofisa wa benki.
Pia Soma
- Profesa Mwafwenga, Mtanzania mwenye digrii saba
- Makonda ataka ujenzi jengo la halmashauri Ubungo kukamilika Desemba 2019
- Bulaya akwamisha kesi ya kina Mbowe
Anadaiwa kutenda kosa hilo Juni 20, 2016 katika Benki ya Wanawake Tanzania (TWB) tawi la Mkwepu lililopo Wilaya ya Ilala.
Anadaiwa akiwa meneja wa tawi hilo akiwa na nia ya uovu alifanya muamala wa uongo kwa kuhamisha Sh120 milioni kutoka akaunti namba 0310137001 ambayo ni ya Florah Lyatuu kwenda akaunti yake namba 0380073121.
Katika shtaka la pili siku na eneo hilo akiwa meneja wa tawi hilo aliiba Sh120 milioni.
Katika shtaka la utakatishaji, Shirika anadaiwa kutenda kosa hilo kati ya Juni 2016 katika benki hiyo.
Siku hiyo, mshtakiwa alijihusisha na muamala wa Sh120 milioni kwa kuruhusu na kufanya malipo kutoka akaunti namba 0380073121 na kuilipa kampuni ya Sekorizi Ltd kupitia hundi tatu zenye namba 000127, 648806 na 1648791 huku akijua kuwa fedha hizo si halali.