Dar es salaam. Kesi ya kuzuia jeshi la polisi kufanya uchunguzi, inayomkabili, Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jamii Forum, Maxence Melo na mwenzake Micke William, imeshindwa kuendelea na utetezi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Wakili wa Serikali Candid Nasua amedai leo Alhamisi Aprili 18, 2019 mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba kuwa shauri hilo limekuja kwaajili ya kusikilizwa lakini Wakili aliyepangiwa shauri hilo ni mgonjwa.
"Shauri limekuja kwa ajili ya kuendelea lakini wakili aliyepangiwa shauri hili anaumwa tunaomba tarehe nyingine kwaajili ya kuendelea na utetezi" amedai Wakili Nasua
Hakimu Simba ameeleza Mahakama zina utaratibu wakumaliza mashauri yake kama wakili husika hayupo mwingine ajipange ili mashauri hayo yakamilike kwa wakati uliopangwa.
Baada ya kueleza hayo, Hakimu Simba ameahirisha shauri hilo hadi Mei 16, 2019 kwaajili ya upande wa utetezi kuleta mashahidi.
Tayari mashahidi wanne wa upande wa mashtaka wameshatoa ushahidi wao dhidi ya washtakiwa hao na Mahakama kuwakuta na kesi ya kujibu.
Katika kesi ya msingi, washtakiwa wanadaiwa kuzuia jeshi la Polisi kufanya uchunguzi, kinyume na Sheria namba 22 (2) cha Sheria ya Makosa ya Mtandano Namba 14 ya mwaka 2015.
Washtakiwa hao wanadaiwa kutenda kosa hilo, kati ya Aprili Mosi, 2016 na Desemba 13, 2016 katika maeneo ya Mikocheni wilayani Kinondoni.