Jeshi la Polisi Mkoani Iringa kwa kushirikiana na Idara ya Uhamiaji mkoani Iringa limewakamata wahamiaji haramu 34 ambao ni raia wa Ethiopia kwa tuhuma za kuingia nchini bila kibali.
Pia, Jeshi hilo linamshikilia dereva wa lori na mkazi wa jijini Dae es Salaam, Maulid Chinunga kwa tuhuma za kuwafirisha wahamiaji hao.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Alhamisi Aprili 28, 2022 Kamanda wa Polisi Mkoani Iringa, Allan Bukumbi amesema wahamiaji hao walikamatwa katika eneo la Confort-Kitonga, wilayani Kilolo wakitokea mkoani Pwani kwenda Tunduma.
“Watuhumiwa wote watafikishwa mahakamani baada ya upelelezi kukamilika,” amesema Bukumbi.
Katika tukio jingine, Kamanda Bukumbi amesema watu sita wanashikiliwa na Jeshi hilo kwa tuhuma za kujihusisha na uhalifu.
“Hawa wamekamatwa kwa nyakati tofauti ndani ya Manispaa ya Iringa wakiwa na vitu mbalimbali vya wizi kama tv, mitungi ya gesi, jiko la umeme, ndoo tupu, viti, magodoro na bidhaa mbalimbali za madukani,” amesema Bukumbi.