JESHI Polisi Mkoa wa Arusha limewakamata wafanyabiashara wawili wakituhumiwa kutumia vibaya silaha kwa kutishiana kuuana kwa risasi kwenye eneo la kituo cha mafuta cha Ngulelo jijini humo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Justine Masejo aliwataja wafanyabiashara hao waliokamatwa juzi kuwa ni Dk Philemon Mollel na William Taitas.
Alisema walikamatwa saa 12:00 jioni katika eneo la tukio baada ya kutishiana kuuana kwa risasi kutokana na mgogoro wa kugombea eneo la ekari
saba.
Hivi karibuni Mahakama Kuu Kanda ya Arusha ilitoa hukumu kuwa eneo hilo si mali ya Mollel ambaye amewekeza kituo cha mafuta na biashara nyingine maeneo ya Ngulelo.
Kamanda Masejo alisema jana kuwa, ugomvi wa watuhumiwa hao uliozua taharuki kwa mamia
ya watu wa eneo hilo waliokimbia ovyo, uliibuka baada ya Mollel kumkuta Taitas akiwaamrisha wafanyakazi wa kituo cha mafuta wakabidhi mali kwa maandishi na waondoke.
Alisema wakati hayo yakiendelea, Mollel alipata taarifa akaenda eneo hilo na kutishia kumpiga risasi Taitas. Kamanda Masejo
alisema Taitas alijibu mapigo kwa kutoa silaha yake ndipo Mollel alipofyatua risasi hewani.
Alisema polisi walifika kwenye eneo la tukio waliwakamata watuhumiwa na wanaendelea kuwahoji na walichukua silaha zao kwa ajili ya uchunguzi.
Wakati huohuo, Jeshi la Polisi mkoani hapa limem-
tia mbaroni mtuhumiwa wa mauaji ya mfanyabiashara wa mchele, Bernadette Chuwa (74) aliyeuawa usiku Aprili 30, mwaka huu kwa kunyongwa nyumbani kwake jijini Arusha.
Kamanda Masejo alimtaja mtuhumiwa kwa jina la Mandela na kwamba awali alifungwa na akaachiwa kwa msamaha wa Rais.