Geita. Mkuu wa mkoa wa Geita, Robert Gabriel amefanya ziara ya kushtukiza katika kiwanda cha uchenjuaji dhahabu na uchomaji wa kaboni cha Ombewa Group kilichopo mjini Geita na kubaini kinaendesha shughuli zake bila kuwa na leseni.
Katika ziara hiyo iliyofanyika leo Jumatatu Juni 25, 2018 saa 1 asubuhi, Gabriel ameagiza kukamatwa raia wanne wa China waliokuwa wakichenjua dhahabu na kuchoma kaboni, jambo aliloeleza kuwa linaitia Serikali hasara.
Mbali na kukamatwa kwa raia hao wa China, pia ameagiza kukamatwa mitambo inayotumika kufanyia shughuli hizo pamoja na mtambo wa CCTV kamera ili kusaidia katika uchunguzi wa wizi wa dhahabu.
Ofisa madini mkoa wa Geita, Ally Said amesema kiwanda hicho bubu alikifunga miezi miwili iliyopita lakini wameendelea kufanya shughuli zao kinyume na sheria.
Amesema kwa mujibu wa sheria za madini kufanya kazi kinyume cha sheria, mhusika hutozwa faini isiyopungua Sh50milioni na mali zake kutaifishwa.