Vijana wawili wamekutwa wakiwa tayari wameshafariki dunia katika bwawa la mradi wa umwagiliaji maji uliopo Kinyasini kisongoni baada ya kutoonekana nyumbani kwao tangu siku ya Jumatano ya wiki hii.
Vijana hao waliofahamika kwa majina ya Khamisi Rajab Mohammed na Nassor Kibwana Khamisi wenye umri wa miaka 25 wote wakaazi wa shehiya ya Chaani kubwa wamekutwa asubuhi ya jana katika eneo hilo wakiwa tayari wameshafariki dunia.
Akizungumza na Zanzibar24 sheha wa shehiya ya chaani kubwa Bw: Abdul-ghafur Ibrahim Ussi amethibitisha kuwa marehemu hao ni wakaazi wa shehiya yake ambao walikuwa wanajihusisha na tabia ya uvutaji wa dawa za kulevya pamoja na ulevi .
Amefahamisha kuwa alipokea taarifa ya kupotea kwa vijana hao kutoka kwa familia za marehemu na asubuhi ya leo ndipo alipopata taarifa yakupatikana kwa miili yao katika bwawa hilo.
Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Kaskazini B Rajab Ali Rajab amesema taarifa za tukio hilo zinasema vijana hao wanasadikiwa kuwa huenda ni miongoni mwa watu waliokuwa wanakimbia Askari wa Jeshi la Polisi lililokuwa linafanya doria katika vijiji vinavyofanya biashara ya ulevi na dawa za kulevya.
Hata hivyo ameitaka jamii kuacha tabia ya kutumia ulevi ili kujiepusha na vitendo kama hivyo ambavyo vinasababisha maafa pamoja na taifa kupoteza nguvu kazi yake.
Maiti hizo zimeokolewa kutoka katika bwawa hilo na kikosi cha zimamoyo na tayari zimekabidhiwa kwa ndugu wa marehemu kwa ajili ya mazishi.
Story na Rauhiya Mussa Shaaban.