WAKAZI wawili wa Dar es Salaam wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, wakikabiliwa na mashitaka ya kusafirisha dawa za kulevya aina ya heroin zenye uzito wa gramu 597.61.
Washitakiwa hao, Ally Ally (32) mkazi wa Kinyerezi na Abubakar Abdallah (28) mkazi wa Kariakoo, walifikishwa mahakamani hapo jana mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Evodia Kyaruzi.
Akisoma hati ya mashtaka, Wakili wa Serikali, Silvia Mintato alidai washitakiwa hao wanakabiliwa na shitaka la kusafirisha dawa za kulevya kosa linaloangukia kwenye sheria ya uhujumu uchumi.
Alidai kuwa, Juni 26, mwaka huu, washitakiwa wakiwa eneo la jengo la J. Mall, wilaya ya Ilala, walikutwa na dawa za kulevya aina ya heroin zenye uzito wa gramu 597.61.
Washitakiwa hao hakutakiwa kujibu chochote kwa sababu Mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi ya aina hiyo.
Upande wa mashitaka ulidai kuwa upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika na kuomba tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa.
Hakimu Kyaruzi aliahirisha kesi hiyo hadi Julai 27, mwaka huu.